Wananchi katika wilaya Kilindi wametakiwa kuzingatia kanuni za usafi wa mazingira ikiwa ni moja ya afua zinazosaidia kupambana na ugonjwa wa Malaria ambao umekuwa ukisababisha athari za kiafya na vifo kwa watanzania.
Wito huo umetolewa jana na Mkuu wa wilaya Kilindi Mh:Sauda Mtondoo wakati alipokuwa akizindua zoezi la kitaifa la ugawaji wa vyanadarua katika ngazi ya kaya ambalo kiwilaya limefanyika katika kijiji cha Kwekivu.
Alisema ugonjwa wa Malaria umekuwa ukileta athari nyingi kiafya ambazo zimekuwa zikisababisha serikali kutumia fedha nyingi kwa ajili ya kugharamia matibabu na ununuzi wa dawa kwa ajili ya tiba kwa wananchi.
Mh:Mtondoo alisema viongozi wa serikali za vijiji vyote wilayani hapa kwa kushirikiana na wananchi wake wanatakiwa kuweka mikakati maalum ya kuhakikisha kila mwananchi anazingatia kanuni za usafi kwa kusafisha mazingira yanayomzunguuka ili kutokomeza mazalia ya Mbu waenezao Malaria.
Akiizungumzia kauli mbiu ya kampeni ya kupambana na Malaria inayosema kabla hujalala chandarua ni lazima Mh:Mtondoo alisema haitakuwa na maana kugawa vyandarua kisha visitumike ipasavyo,hivyo wananchi wote wanapaswa kutekeleza kwa vitendo kauli mbiu hii kwa kuhakikisha wanatumia vyandarua wakati wote wa kulala.
Aliishukuru serikali awamu ya tano inayoongozwa na Mheshimiwa Dk. John Pombe Magufuli kwa kuhakikisha inalinda afya za wananchi wake kwa kuendesha zoezi maalum la ugawaji wa vyandarua katika ngazi ya kaya na kuongeza kuwa uamuzi wa serikali wa kuwekeza katika kinga dhidi ya ugonjwa wa Malaria ni wa muhimu na kusisitiza matumizi sahihi ya vyanadarua hivyo.
Alitoa onyo kwa wananchi ambao watatumia vyandarua hivyo kinyume na inavyotarajiwa kama vile kufugia vifaranga na kwamba hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi ya wananchi hao kwani serikali imetumia fedha nyingi kununua vyandarua hivyo
Zoezi la ugawaji wa vyanadarua ngazi ya kaya katika Wilaya Kilindi limezinduliwa kwa Mh:Mkuu wa wilaya kugawa vyandarua 15 katika makundi ya walemavu,wajawazito,watoto na wazee.
Zaidi ya kaya 80,000 zinatarajiwa kupata vyandarua katika zoezi linalotarajiwa kuendeshwa wilaya nzima ya Kilindi.
Habari Na: Modi Mngumi
Copyright ©2018 Kilindi DC . All rights reserved.