Na Ulirch P. Laswai
Baraza la Madiwani la Halmashauri ya Wilaya ya Kilindi limeendelea na zoezi la kutatua Migogoro mbalimbali ya Ardhi katika ngazi za Kata na Vijiji. Baraza hilo la Madiwani linalenga kumaliza kabisa migogoro ya Ardhi iliyopo baina ya kata kwa kata na vijiji kwa vijiji ili kusaidia wananchi wa Kilindi kuondokana na kero hiyo.
Akizungumza katika Baraza la Madiwani lililofanyika katika Ukumbi wa Halmashauri Novemba 22 mwaka huu, Mkurugenzi Mtendaji, Ndugu Gracian Max Makota amewataka waheshimiwa Madiwani na viongozi wa ngazi za Kata na Vijiji kumaliza migogoro ya ardhi iliyopo kwenye maeneo yao ya uongozi kwa kutumia taratibu, kanununi na sheria za ardhi na kutumia busara katika kupata suluhisho la migogoro hiyo iliyodumu kwa muda mrefu.
“Nguvu nyingi zimetumika, fedha pamoja na busara katika kutatua migogoro ya ardhi Kilindi bila ya kupata suluhisho,badala ya kutumia nguvu hizo kwa kufanya shughuli za maendeleo kama ujenzi wa madarasa, kwani chembechembe za migogoro hii ipo katika ngazi ya kata, sasa tunaweka azimio la kumaliza migogoro yote ya ardhi katika kata mnakotokea” Alisema Mkurugenzi Mtendaji
Makota amekuwa akifanya mawasiliano na baadhi ya Watendaji wa vijiji mara kwa mara kila inapotokea migogoro ya ardhi pamoja na kuwatumia waheshimiwa madiwani katika kutoa elimu ya kutafuta shuluhisho la migogoro ya ardhi pamoja na wataalam wa Ardhi ngazi ya wilaya, ngazi ya Mkoa na hata Wizara pasipo kumaliza migogoro ya ardhi Kilindi, badala yake ikagundulika kuwa matatizo hayo yanasababishwa na viongozi katika ngazi za kata na vijiji, hicho ndicho kilichopelekea Mkurugenzi Mtendaji kutoa agizo kwa baraza la Madiwani kwenda kumaliza migogoro hiyo katika ngazi za kata.
Kwa upande wa Waheshimiwa Madiwani waliafiki kwa pamoja kuwa suala la kutatua migogoro ya ardhi nilalazima na kwamba wapotayari kulitekeleza kwa mujibu wa kanuni, taratibu na sheria za ardhi zilivyo na kwa kushirikiana na viongozi waliopo katika ngazi za kata na vijiji ili kuwasaidia wananchi wa Kilindi kuondokana kabisa na changamoto hiyo, lakini baadhi yao walisema pindi tatuzi zikiwa zinafanyika kama kutakuwa na ulazima wataomba msaada wilayani hasa kwa migogoro baina ya kata kwa kata na ile ya kati ya Kilindi na vijiji vya wilaya nyingine.
Mwenyekiti wa chama cha Mapinduzi (CCM) wa Wilaya ya Kilindi Mhe.Bakari H.Kingalangala naye aliafikiana na wajumbe wa Baraza la Madiwani kuhusu azimio la kutatua migogoro katika ngazi za kata na vijiji, lakini pia alizungumzia chanzo cha migogoro ya Ardhi Kilindi kuwa inasababishwa na wenyeviti wa vijiji wanaouza maeneo kiholela kwa tamaa za kupata fedha na kwa upande mwingine ni hata wataalam wa ardhi kwa kuwa wanatumia ramani za vijiji ambazo hazikuwahusisha wananchi wakati zinaandaliwa Mfano ni ramani ya vijiji ya mwaka 2007 iliyoandaliwa na wizara ya ardhi na makazi.
Copyright ©2018 Kilindi DC . All rights reserved.