Na Modi Mngumi
Wakazi wa kata ya Pagwi katika Halmashauri ya Wilaya Kilindi wameanzisha mpango wa stoo ya matofali kwa lengo la kurahisisha uchangiaji wa ujenzi wa miundombinu mbalimbali ya maendeleo ya ujenzi.
Wakizungumza na Mkuu wa Wilaya Kilindi Mh:Abel Yeji Busalama wakati wa ziara yake ya kuhamasisha maendeleo na kusikiliza kero za wananchi wakazi hao walisema kwa kuanza wameamua kufyatua tofali 67,000 ambazo ni kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha Afya.
Walisema katika mpango wao wataendelea kufyatua tofali nyingi zaidi kwa ajili ya kujiandaa na ujenzi wa madarasa hasa kwa ajli ya vijana wanaotarajiwa kujiunga na kidato cha kwanza mwakani.
Walisema katika mpango huo wa stoo ya matofali kila watu wawili wanatakiwa kutoa mfuko mmoja wa Saruji na Tsh 6,500/= za kufyatulia tofali.
Akizungumza na wananchi hao Mh.Busalama aliwapongeza kwa ubunifu huo na kuwataka wakazi wa maeneo mengine katika wilaya Kilindi kuiga mfano huo ambao utasaidia kurahisha ujenzi wa aina mbalimbali pale wananchi watakapohitajika kuchangia nguvu zao.
Akiwa katika ziara hiyo ya kuhamasisha maendeleo Mkuu wa Wilaya alitembelea miradi ya maji ya kata ya Kwekivu,Kikunde na Chamtui ambapo alitoa wito wa kuundwa haraka kwa Bodi za maji ambazo zitasaidia miradi hiyo kuwa endelevu na kutatua changamoto zake.
Alisema Bodi za maji zitakuwa ni msaada mkubwa katika kusimamia miradi hiyo ambayo inakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo mapato kidogo na kuongeza kuwa Bodi hizo zitasaidia miradi hiyo kuongeza mapato na kuleta tija kama ilivyokusudiwa.
Akiwa katika kata ya Kikunde ambako alizungumza na wananchi Mh.Busalama aliwataka wananchi kujiunga na mfuko wa Afya ya Jamii Ulioboreshwa (ICHF) pamoja na kuwa wabunifu wa kufanya miradi mbalimbali ili kupambana na umaskini wa kipato katika kaya.
Mh:Busalama katika ziara hiyo pia alikagua ujenzi wa mabweni na maabara katika shule ya sekondari Kikunde.
MWISHO
Halmashauri ya wilaya ya Kilindi
Copyright ©2018 Kilindi DC . All rights reserved.