Mkuu wa Wilaya ya Kilindi Mhe. Sauda Salumu Mtondoo amewataka watumishi wa idara ya Afya Wilayani Kilindi kutunza siri za wateja wanaojitokeza kupima maambukizi ya virusi vya UKIMWI ili kuongeza mwamko wa upimaji Afya.
Aidha amewataka watumishi wa Idara ya Afya kuonyesha upendo na kuwaelimisha wananchi kuhusu umuhimu wa kuhudhuria kliniki kwa wakati na ufuasi mzuri wa dawa .
Mhe. Mtondoo amesema hayo alipokuwa katika maadhimisho ya siku ya UKIMWI Duniani ambayo yamefanyika Kiwilaya kata ya Lwande leo tarehe 01.12.2020.
Madhimisho haya yaliongozwa kwa kauli mbiu ya “Mshikamano wa Kimataifa tuwajibike kwa pamoja”. yalihusisha asasi za Serikali na binafsi pamoja na wananchi wa Wilaya ya Kilindi ambapo mgeni rasmi alikuwa ni Mkuu wa Wilaya ya Kilindi Mhe. Sauda Salumu Mtondoo.
“Dumisheni ushirikiano kati ya Halmashauri, asasi za kijamii na mashirika yasiyokuwa ya kiserikali katika kupunguza maambukizi mapya ya VVU.” Alisema Mhe. Mtondoo alipokuwa akisisitiza mambo ya kuzingatia ilikupunguza maambukizi ya virusi vya UKIMWI.
Aidha kiwango cha maambukizi kiwilaya kutokana na upimaji uliofanyika Januari hadi Oktoba 2020 Jumla ya watu 84,869 kati yao wanaume 38,636 na wanawake 46,233 walipima VVU na waliogundulika kuwa na maambukizi ni 715 kati yao wanaume ni 262 na wanawake 453 ambapo kiwango cha maambukizi ni sawa na asilimia 1.0 ikimaanisha kuwa katika kila watu 100 mtu mmoja ana maambukizi ya VVU.
Hata hivyo amewataka wazazi na walezi kuhakikisha Vijana na Wanafunzi wanapatiwa stadi za maisha zitakazowawezesha kuchelewa kuanza kujamiana, Kuendelea kutoa elimu kwa jamii kuhusu athari za unyanyapaa na ubaguzi kwa watu wanaoishi na VVU na UKIMWI.
Imetolewa na:
Ndg. Ulirch Laswai na Samwel Mwantona
Kitengo cha Habari na Mawasiliano (W)
Copyright ©2018 Kilindi DC . All rights reserved.