Mkuu wa wilaya Kilindi Mh: Sauda Mtondoo amewataka watumishi wa serikali wilayani hapa kutokuwa chanzo cha kusababisha kero kwa wananchi na badala yake wawe sehemu ya kutatua kero hizo.
Mh:Mkuu wa wilaya alitoa agizo hilo jana wakati alipokuwa akizungumza na watumishi katika kikao kazi kilichofanyika katika ukumbi wa Halmashauri ya wilaya Kilindi.
Alisema watumishi wa serikali katika ngazi za vijiji,kata na tarafa ni wawakilishi wa viongozi katika ngazi ya wilaya kwani wao wapo karibu zaidi na wanachi,hivyo kero zao zinapaswa kusikilizwa na kutatuliwa mapema ili zisikomae na hatimaye jamii kukata tamaa na kupoteza imani na serikali yao.
Mkuu huyo wa wilaya alisema zipo kero nyingi za wananchi ikiwemo migogoro ya ardhi ambayo watendaji wa vijiji na halmashauri zao za vijiji wasigeuze migogoro hiyo kuwa sehemu ya miradi binafsi na serikali haitasita kuwachukulia hatua kali za kisheria watendaji wote watakaokiuka taratibu za kazi na maadili ya kiutumishi.
Mh:Mtondoo alisema serikali za vijiji zifuate taratibu na miongozo ya ugawaji wa maeneo kwa wananchi ili kuepuka migogoro na kero kwa jamii na kuwataka watendaji kubadilika katika utekelezaji wa majukumu yao.
Katika kikao hicho watendaji hao katika ngazi ya vijiji,kata na tarafa walipatiwa elimu na miongozo mbalimbali ikiwemo masuala ya ardhi,manunuzi,mabaraza ya kata,ukaguzi na misitu na kupata fursa ya kuuliza maswali na kupatiwa majibu na ufafanuzi ili kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao.
Kikao kazi hicho kilishirikisha watendaji wa vijiji,kata na maafisa tarafa kutoka katika vijiji,kata na tarafa za Halmamashauri ya wilaya Kilindi.
NA:MODI MNGUMI
Copyright ©2018 Kilindi DC . All rights reserved.